Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA

ISO 9001:2015 Imethibitishwa Kutoa Huduma za Hali ya Hewa kwenye Usafiri wa Anga

WADAU WAJENGEWA UELEWA WA HUDUMA ZA HALI YA HEWA ZINAZOTOLEWA NA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA.

News Image

WADAU WAJENGEWA UELEWA WA HUDUMA ZA HALI YA HEWA ZINAZOTOLEWA NA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA.

 

Dodoma

Wadau kutoka sekta mbalimbali wamejengewa uelewa wa huduma za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kupitia warsha ya siku mbili iliyofanyika katika Hoteli ya Best Western, Dodoma.

Warsha hiyo ilifunguliwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a, tarehe 22 Januari ambapo alisema warsha hiyo inalenga kuimarisha matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii, na hivyo kuongeza ufanisi na tija katika shughuli hizo.

Katika warsha hiyo, wataalamu wa TMA waliwasilisha na kutoa ufafanuzi wa huduma mbalimbali zinazotolewa na TMA, ikiwemo utabiri wa kila siku na tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa.  Wataalamu walianisha pia matakwa ya kisheria  kwa WADAU kutumia na kuzingatia taarifa za hali ya hewa  katika shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo katika sekta ya Ujenzi, usafiri wa Anga na Maji.

Wadau pia wamepata fursa ya kujifunza  na kupata taarifa kuhusu mwelekeo na kasi ya mabadiliko ya hali ya hewa nchini Tanzania, wajibu wa jamii katika kukabiliana na athari zake, pamoja na masuala ya usawa wa kijinsia na ujumuishaji wa makundi maalum katika juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

Warsha hiyo iliitimishwa rasmi, leo  tarehe 23 Januari 2026, na Mkurugenzi wa Udhibiti na Ubora wa Huduma za Hali ya Hewa, Dkt. Georfrid E. Chikojo, akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TMA. Kabla ya kufunga warsha hiyo, Dkt. Chikojo aliwashukuru wadau wote kwa ushiriki wao na mchango wao katika kuimarisha huduma za hali ya hewa nchini  huku akisisitiza wadau na waandishi wa habari  kuelimisha jamii na kusimamia sheria ya mamlaka ya hali ya hewa nchini.